Kondakta wa daladala, Hamim Seif (42)
mkazi wa Mwananyamala Ujiji, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu
Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka la kutishia kumuua Rais John Magufuli kwa
maneno.
Seif alipandishwa kizimbani mahakamani
hapo jana mchana na kusomewa shtaka hilo na Wakili wa Serikali Mwandamizi,
Kenneth Sekwao.
Mshtakiwa huyo alikana shtaka hilo na
Hakimu Mkazi, Hellen Liwa alisema kuwa dhamana ya mshtakiwa huyo iko wazi na
alitakiwa kuwa na wadhamini wawili, kutoka taasisi ya Serikali inayotambulika,
ambaye atasaini hati ya dhamana ya Sh2 milioni.
Licha ya dhamana yake hiyo kuwa wazi,
mshtakiwa huyo alishindwa kukamilisha masharti hayo kwani baada ya kusomewa
mashtaka alipoulizwa kama alikuwa na wadhamini alishindwa kuwapata.
Akimsomea shtaka linalomkabili, Wakili
Sekwao alisema kuwa mshtakiwa huyo alitenda kosa hilo Machi 10 mwaka huu katika
baa ya Soweto, Makumbusho wilayani Kinondoni kinyume cha kifungu cha 89 (2) (a)
na kifungu cha 35 cha Sheria ya Kanuni za Adhabu.
Wakili Sekwao alisema akiwa katika baa
hiyo, mshtakiwa alitishia kumuua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk
John Magufuli kwa maneno kwa njia ya kujitoa mhanga.
“Kwa haya mambo anayoyafanya Rais
Magufuli, mimi nimo tayari kujilipua kwa kujitoa mhanga ili kumuangamiza,”
alisema Wakili Sekwao akimnukuu mshtakiwa huyo.
Hata
hivyo, Wakili Sekwao alisema upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na akaomba
tarehe nyingine kwa ajili ya kesi hiyo kutajwa.
No comments:
Post a Comment