Tunakupa habari motomoto na uchambuzi wa kina

Search This Blog

Breaking

Serikali kuja na mpango wa kodi ya nyumba kulipwa mwezi mmoja mmoja

TANGAZA NASI HAPA


2016-04-20

BUNGENI: WATUHUMIWA 135 WAKAMATWA KWA MAKOSA YA MAUAJI YA VIKONGWE NCHINI


Watuhumiwa 135 wamekamatwa kwa makosa ya mauaji ya vikongwe nchini, kati ya Julai mwaka jana na Machi mwaka huu.

Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Masauni, alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Faida Mohamed Bakari (CCM).

Faida alitaka kufahamu hatua zinazochukuliwa na Serikali kukomesha mauaji hayo na msaada wanaotoa kwa wanawake wanaotumia kuni kupikia, ambayo ni moja ya chanzo kinachosababisha macho kuwa mekundu na hivyo wauaji kuwaua.

“Watu wamekuwa wakiuawa kwa kufukiwa wakiwa hai kwa sababu ya macho mekundu, yanayotokana na moshi wa kuni au kupika kwa kutumia kinyesi cha ng’ombe,” alisema.

Masauni alisema licha ya watuhumiwa hao kukamatwa, kuna kesi 222 zinazoendelea mahakamani.

“Serikali inafanya jitihada mbalimbali ikiwamo kuhamasisha utengenezaji majiko sanifu, kupeleka gesi na umeme vijijini,” alisema. 

Katika swali la msingi, Mbunge wa Viti Maalumu, Tauhida Cassian Galloss (CCM), alitaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kunusuru vikongwe.

Masauni alisema Polisi imeweka mikakati mbalimbali ya kupambana na mauaji hayo, ikiwamo kufanya operesheni na misako ya mara kwa mara kuwabaini waganga wa jadi wanaojihusisha na upigaji ramli chonganishi na wasiofuata taratibu za sheria. Pia, alitaka jamii kutoa ushirikiano.

No comments:

Post a Comment

Tunakupa habari motomoto na uchambuzi wa kina