Mkuu wa wilaya ya Mkalama mh Christorher Ngubiagai |
MKUU wa Wilaya ya Mkalama mkoani Singida, Christopher Ngubiagai ameagiza
Mkuu wa Shule ya Sekondari Chemichem wilayani humo, Juma Makoro kukamatwa na
kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kutokana na tuhuma za kufanya mapenzi na
wanafunzi wake.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya amemwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri
hiyo kumwandikia barua ya kumsimamisha kazi mwalimu huyo kupisha uchunguzi wa
tuhuma zinazomkabili .
Vile vile ameagiza Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(Takukuru) kufuatilia suala hilo. Ngubiagai alitoa agizo hilo juzi wakati wa
kikao cha pamoja baina ya Watendaji wa Vijiji, Kata, Tarafa na Waratibu Elimu
wa kata wa halmashauri hiyo na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya
kilichofanyika mjini Nduguti.
Alisema kuwa vitendo viovu vya mkuu huyo wa shule viligundulika baada ya
wanafunzi kulalamika kwa wazazi wao juu ya vitendo hivyo na wazazi kuamua
kulifikisha suala hilo kwenye mamlaka za juu. “Haiingii akilini jinsi ambavyo
mwalimu huyu alivyokuwa akiwadhalilisha wanafunzi wake wa kike kijinsia.
Tunaambiwa mwanafunzi akimpelekea madaftari kabla hajayapokea anamwambia
mwanafunzi ambusu kwanza,” alisema Ngubiagai huku akionesha kuudhiwa na jambo
hilo. “Mwalimu ni mzazi wa pili, ndivyo tunavyoamini.
Sasa huyu mzazi akifikia hatua hiyo huyo mwanafunzi atapata malezi ya
aina gani? Ni jambo la aibu sana na ni kinyume na maadili ya taaluma ya ualimu.
Kamwondoeni huyo wanafunzi wasome kwa amani,” aliagiza.
No comments:
Post a Comment