Tunakupa habari motomoto na uchambuzi wa kina

Search This Blog

Breaking

Serikali kuja na mpango wa kodi ya nyumba kulipwa mwezi mmoja mmoja

TANGAZA NASI HAPA


2016-03-21

WATOTO WANNE WANAJISIWA MWAKA MZIMA.


watoto hao wanaosoma darasa la tatu katika Shule ya Msingi ya Msaranga  Manispaa ya Moshi
 Watoto wanne wa kike wenye umri wa miaka minane wamebainika kunajisiwa kwa karibu mwaka mzima huku vijana wawili wanaowafanyia vitendo hivyo wakiwalipa Sh500 kila mmoja.

Habari zinasema watoto hao wanaosoma darasa la tatu katika Shule ya Msingi ya Msaranga  Manispaa ya Moshi, wamekuwa wakienda kufanyiwa vitendo hivyo asubuhi kabla ya kuingia darasani.
Uchunguzi wa madaktari wa hospitali ya rufaa ya Mkoa Kilimanjaro ya Mawenzi umethibitisha watoto hao kuingiliwa kwa kunajisiwa na kuambukizwa magonjwa ya zinaa.
Watoto hao wamekuwa wakifanyiwa vitendo hivyo kati ya saa 12.30 na saa 1.30 asubuhi na baadaye hutakiwa kurudi saa nne wakati wa mapumziko kuchukua Sh500 kama malipo ya ujira wa kazi hiyo.
Mkazi mmoja wa Msaranga ambaye hakutaka jina lake kutajwa, alishuku mwenendo usio wa kawaida wa mjukuu wake ambaye ni miongoni mwa watoto hao.
Ilikuwa kati ya saa 12.30 au saa 1.00 asubuhi nilikuwa natoka misa ya asubuhi nikakutana naye na wenzake wanavuka barabara kwenda upande tofauti na ilipo shule,” alisema mzee huyo.
Nilipomuuliza unakwenda wapi akasema mwalimu amewatuma madekio,  lakini nikamuona anatetemeka. Nikamuamuru arudi shule mara moja. Mie nikaendelea na safari yangu lakini roho ikakataa.”
Mzee huyo alisema saa mbili asubuhi siku hiyohiyo, alikwenda shuleni kukutana na mwalimu mkuu lakini alikutana na mwalimu wa zamu na kumueleza shaka yake.
Kwa mujibu wa mzee huyo, mwalimu aliahidi kuchunguza jambo hilo, lakini siku hiyo mjukuu wake aliporudi nyumbani alimuuliza na baada ya kumchapa kidogo akaeleza kila kitu.
Siku iliyofuata mzee huyo alirudi shuleni na kumueleza mwalimu mkuu taarifa zile naye aliita walimu wenzake na kumuita mtoto huyo na kumuuliza kama ni kweli alichoeleza babu yake.
Mwalimu mkuu akamwambia usiposema ukweli nitakuadhibu, ndipo akasema huwa wanakwenda kwa wavulana fulani kufanya hayo mambo na akawataja wenzake watatu anaokwenda nao,” alisema.
Mlezi huyo alidai mbele ya walimu alieleza kuwa huwa wanakwenda huko asubuhi na kufanyiwa vitendo hivyo kwa zamu katika chumba kimoja halafu hutakiwa kurudi saa nne asubuhi kuchukua Sh500.
“Watoto wawili akiwamo huyu mjukuu wangu walikiri na kuwataja kwa majina vijana na kutueleza fulani huwa anatufanya mbele na fulani anatufanya nyuma. Wawili waligoma kueleza,” alisema.
“Wametwambia saa nne wakati wa mapumziko ndiyo wanakwenda kuchukua hiyo 500 kila mmoja halafu siku nyingine hurudi saa nane mchana,” alisema.
Mtoto huyo alipohojiwa na mwandishi wetu alitoa maelezo yanayofanana na ya babu yake na kuwataja  majina vijana hao.
Alhamisi iliyopita, majirani walihamasishana kwenda kwenye nyumba husika eneo la Lombeta, umbali wa mita 800 kutoka shuleni hapo, lakini kabla ya kufanya hivyo walimpigia simu mwenyekiti wa mtaa ambaye aliwashauri waende polisi.
“Tulipofika Polisi Majengo tukapewa PF3 (fomu ya polisi) tukaenda na wale watoto wawili hadi kwa daktari Mawenzi na baada ya kuwapima alishtuka sana,” alisema mmoja wa majirani hao, Lilian Kisanga.
Kisanga alisema daktari aliwashauri warudi siku inayofuata kwa ajili ya watoto kupimwa kama wameambukizwa magonjwa ya zinaa na vipimo vilithibitisha watoto hao kuambukizwa.
“Ijumaa tulikwenda na polisi kwenye ile nyumba tukafanikiwa kumkamata kijana mmoja ambaye watoto wanamtambua kwa sura na jina,” alisema Lilian.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa alithibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa mmoja wa tukio hilo.
“Ni kweli kuna shauri hilo limefunguliwa na tayari tumemkamata mmoja wa watuhumiwa na tunaendelea kumtafuta mwingine anayetajwa na watoto hao,” alisema.
Mutafungwa alisema kutokana na uzito wa kosa hilo ambalo likithibitika mahakamani adhabu yake ni kifungo cha maisha, ameagiza dhamana ya mtuhumiwa izuiliwe kwa sasa.
“Ni matukio mabaya na machafu ambayo mtu ukiyasikia yanaumiza sana. Tayari nimeagiza jalada lihamishwe kutoka Majengo lipelekwe Dawati la Jinsia,” alisema Mtanfungwa na kuongeza:
“Tunawaomba wananchi wenye taarifa za mahali alipo mtuhumiwa wa pili watuletee ili akamatwe na yeye mwenyewe huko aliko ajisalimishe.”
Taasisi mbalimbali za kutetea haki za wanawake na watoto mkoani Kilimanjaro zimeapa kulivalia njuga suala hilo na leo watapiga kambi kituo kikuu cha kati cha Polisi kufuatilia sakata hilo.
Mkurugenzi wa taasisi ya Kilimanjaro Women Information Exchange and Consultancy Organisation (Kwieco), Elizabeth Minde aliwataka polisi kuchunguza tukio hilo kwa uzito unaostahili.
“Tunataka uchunguzi wa kina ufanyike ni tukio baya ambalo limetushtua sisi kama wazazi. Uko nyumbani unaamini mtoto kaenda shule kumbe anafanyiwa ufedhuli wa aina hiyo,” alisema.
Aliwataka wazazi kujenga utamaduni wa kuwachunguza watoto wao mara kwa mara kila wanaporudi kutoka shuleni ili kubaini kama kuna mabadiliko ya kitabia au kutokuwapo shuleni kwa kipindi fulani. Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi, Jeshi Lupembe aliahidi kwenda katika shule hiyo leo kuchunguza suala hilo.
Tukio hilo linafanana kwa kiasi na lile la mwanamuziki, Nguza Viking “Babu Seya” na mwanaye, Johnson Nguza “Papii Kocha” wanaotumikia kifungo cha maisha jela baada ya kutiwa hatiani.

Wanamuziki hao, walihukumiwa mwaka 2004 baada ya kupatikana na hatia ya kubaka na kunajisi watoto 10 wenye umri wa kati ya miaka sita na minane wa Shule ya Msingi Mashujaa, Dar es Salaam na sasa wamekata hukumu katika Mahakama ya Afrika Mashariki kupinga hukumu hiyo.

No comments:

Post a Comment

Tunakupa habari motomoto na uchambuzi wa kina